RAIS MSTAAFU JAKAYA KIKWETE ATUNUKIWA TUZO YA UONGOZI WA KISIASA NA UTETEZI




Shirika lisilo la  Kiserikali    la Speak  Up for Afrika   limemtunukia tuzo, Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete kutokana na uongozi wake wa kisiasa na utetezi wake  kwa  makundi ya jamii yaliyo katika mazingira magumu hususani wanawake na watoto.
 
Utoaji wa  Tuzo hiyo  ya  uongozi wa kisiasa na utetezi , umekwenda sambamba na   hafla ya  miaka mitano ya kuanzishwa kwa  Taasisi ya Speak up  Afrika. Hafla  hiyo iliyofanyika jana Alhamisi Jijini New York   ilikuwa  pia  ni sehemu ya kuhamasisha uchangiaji   wa shughuli za  Taasisi hiyo.
 
Mchango ambao umetambuliwa na  Speak Up  Afrika,   taasisi ambayo imekuwa ikifanya kazi  kwa Karibu na Rais Mstaafu Kikwete, ni  katika maeneo ya  upelekaji na usambazaji wa huduma za msingi za afya hususani afya ya mama na mtoto,  udhibiti wa  ugonjwa  wa malaria kupitia kampeni  ya malaria haikubaliki ,usambazaji wa vyandarua  vyenye viatilifu, kampeni ya  lishe bora, na  kampeni ya   chanjo kwa watoto.
 
Pamoja  na  kutambua  juhudi za   Rais Mstaafu  Kikwete katika  kuyasemea maeneo hayo,  Taasisi hiyo kupitia  Mkurugenzi wake  Mtendaji Bi. Kate Campana pia imemtambua  kama kiongozi ambaye    amekuwa mstari wa mbele  wa kulisema Bara la Afrika kila  mara alipopata  fursa  ya  kufanya hivyo wakati akiwa madarakani na hata baada ya kustaafu.
 
Rais kikwete ameelezwa katika hafla hiyo iliyowashirikisha  wadau wa kada mbalimbali, kama kiongozi wa kisiasa ambaye amezigusa nyoyo za watu wengi kujitolea kwaajili ya watu wenye mahitajio ya kupata huduma za msingi za kijamii ambazo  au wameshindwa kuzipata kutokana na kipato kidogo au haziwafikii kabisa.
 
Akipokea  Tuzo hiyo, Rais  Mstaafu Kikwete , amesema Tuzo hiyo ni ya watoto wote  waafrika ambao ndio  waliomfanya asimame   mbele ya wageni waalikwa.
 
“ Ni kwa sababu yenu ndio sababu nimetenga muda wangu  baada ya kustaafu kusukuma mbele agenda ya  kuboresha maisha yenu. Ninafanya hivyo kwasababu makuzi yangu yalikuwa kama  ya mtoto yeyote yule wa  kiafrika, nimeyaishi maisha  wanayo ishi. Na kwa hiyo ninaelewa fika  hamu na kiu yao ya kuwa  na maisha bora na afya njema”. Akasema Kikwete na kushangiliwa na wageni waalikwa.
 

No comments:

This Website Is Developed & Maintained By Jesse. Powered by Blogger.