KAMANDA SIRO AMPA FREEMAN MBOWE MPAKA KESHO KUTII WITO WA MAKONDA



Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Siro amesema endapo Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe hataripoti kituoni kesho (saa 48 tangu jana), atatafutwa kwa namna ambayo jeshi hilo litaona inafaa.

Mbowe ni miongoni mwa watu mashuhuri waliotajwa hivi karibuni katika orodha ya watu 65 ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda wanaodaiwa kujua taarifa za wanaojihusisha na dawa za kulevya. 

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamishna Siro alisema Mbowe kupitia kwa baadhi ya viongozi aliwajulisha angeripoti Kituo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam, Jumatano ya Februari 15, lakini alikuwa hajaripoti hadi jana 

“Jumatatu asiporipoti kutakuwa hakuna namna ya kulizuia tena Jeshi la Polisi kutafuta namna ya kumuhoji,” alisema. 

“Mheshimiwa Mbowe tunamheshimu sana kama kiongozi wa chama kikubwa cha siasa na hata akiwa bungeni ameonekana akipinga kwa nguvu suala la dawa za kulevya na anasikitika kuona vijana wa Kitanzania wanateketea. 

Image result for mbowe

"Asitafute namna nyingine, tunamuhitaji kwa ajili ya kumuhoji kutokana na hizi tuhuma za dawa za kulevya,” alisema Siro. 

Alisema kiongozi kama Mbowe hatakiwi kuwa mtu wa kuta- futwa.”Jeshi la Polisi lisingependa kuwa na mvutano na yeye, najua anajua kuwa tunamtafuta. 

"Jana (juzi) tumejitahidi kumtafuta kwa simu hajapatikana, tumekwenda nyumbani kwake hatujampata na hata tulipokwenda mahali ambapo inasemekana anaishi sasa hatukumpata, alisema. 

Hata hivyo, Februari 10 akiwa mjini Dodoma, Mbowe alisema hatafika polisi kwa kuitwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda lakini yupo tayari kutoa ushirikiano kwa vyombo vya dola endapo utaratibu wa kisheria utafuatwa. 

No comments:

This Website Is Developed & Maintained By Jesse. Powered by Blogger.