CAG: DENI LA TAIFA LIMEONGEZEKA KWA ASILIMIA 27 ( JUNE 30/2014 - JUNE 30/2015)





MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ametoa ripoti ya ukaguzi wa hesabu ya mwaka 2014/15 iliyoibua kasoro nyingi kwenye taasisi na mashirika mbalimbali ya serikali huku halmashauri zikibainika kuwa na ‘madudu’ mengi.
Ripoti hiyo inaonesha kati ya halmashauri 164 zilizokaguliwa, 47 pekee ndizo zimepata hati safi, nyingine zilizobakia zina hati zenye mashaka, zisizoridhisha na chafu. Kwa upande wa mashirika ambayo ripoti hiyo imeyagusa, Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA) limebainika mauzo ya hisa zake yalikuwa batili, hivyo CAG ameshauri lirudi chini ya usimamizi wa serikali hadi hapo mgogoro wa mgawanyo wa hisa utakapotatuliwa.
UTATA JUU YA DART
Kuhusu Wakala wa Usafiri wa Mwendo wa Haraka Dar es Salaam (DART), ripoti ya CAG imebaini kuwa kwa mwaka wa fedha 2014/15 wakala huyo aliingia mkataba na UDA-RT wa kutoa huduma ya usafiri wa mpito wa kuendesha mabasi 76 kulingana na vigezo vilivyoainishwa kwenye mkataba.
Lakini, Sheria ya Manunuzi ya Umma, mkataba huo ulitoa ongezeko la ununuzi wa mabasi na kufikia 84 ili kulingana na matakwa ya DART. Hata hivyo kwenye ukaguzi wa hesabu zao, CAG alibaini kuwepo na ununuzi wa mabasi 140 ambayo ni sawa na ongezeko la mabasi 56 yasiyo ndani ya mkataba.
WATUMISHI HEWA NA MISAMAHA YA KODI
Aidha, ripoti hiyo imepigilia msumari kwenye suala la watumishi hewa na kusema tatizo hilo limekuwa sugu na serikali za mitaa zinaongoza kwa kulipa mishahara watumishi waliofariki na waliotoroka huku Sh bilioni 2.7 zikiwa zimetumika mwaka wa fedha 2014/15 kwa malipo hayo.
Jambo lingine ambalo limejitokeza kwenye ripoti ya CAG, ni utoaji wa misamaha ya kodi kwa kiwango cha juu huku ikionesha Sh trilioni 1.6 sawa na asilimia mbili ya pato la ndani la taifa, zilisamehewa katika kipindi kilichoishia Juni 30, 2015.
MADUDU KATIKA HALMASHAURI
Alisema kwa mwaka unaoishia Juni 30 ,2015, jumla ya hati za ukaguzi 465 zilitolewa kwa Serikali Kuu, Serikali za Mitaa na mashirika ya umma. Ripoti imeonesha kuwa mashirika ya umma na Serikali Kuu yamefanya vizuri kwa kupata hati nyingi safi, huku zile za mashaka zikiwa chache.
Aidha hakuna hati mbaya wala isiyoridhisha. Akifafanua alisema katika ukaguzi huo, halmashauri ndizo zinaongoza kwa kufanya vibaya . Kati ya halmashauri 164 zilizokaguliwa, 47 pekee ndizo zimepata hati safi, nyingine zilizobakia ni zenye mashaka, zisizoridhisha na chafu.
MISAMAHA YA KODI
Wakati huo huo, akizungumzia misamaha ya kodi kwa kipindi kilichoishia Juni 30, 2015, Profesa Assad alisema ripoti yao inaonesha kuwa kiasi cha misamaha kilichotolewa ni Sh trilioni 1.6 sawa na asilimia mbili ya pato la ndani la taifa.

Kiwango hicho kwa mujibu wa Profesa Asaad, ni cha juu ikilinganishwa na lengo la serikali la kupunguza misamaha hiyo isizidi asilimia moja ya pato la taifa.
Katika misamaha hiyo, pia kuna utata kwenye mafuta yenye dhamana ya kodi ya Sh bilioni tano ambayo yalionekana kwenye mfumo wa forodha wa (TANCIS) kuwa yamesafirishwa nje kupitia nchini lakini hakuna ushahidi wa hilo.
DENI LA TAIFA
Akizungumzia deni la taifa, Profesa Asaad alisema hadi kufikia Juni 30, mwaka 2015, deni la taifa lilikuwa Sh trilioni 33.54. Deni la ndani lilikuwa Sh trilioni 7.99 na deni la nje likiwa Sh trilioni 25.5 hivyo jumla ya deni lote likiongezeka kwa asilimia 27 ikilinganishwa na deni lililoishia Juni 30, mwaka 2014,hivyo ameishauri Serikali kuongeza jitihada za kukusanya kodi ili kulipa madeni.

No comments:

This Website Is Developed & Maintained By Jesse. Powered by Blogger.